Pixabay
02 Sep 2021 Toleo la habari Air quality

Moja kati ya nchi tatu ulimwenguni haina viwango vyovyote vilivyoidhinishwa kisheria kuhusu ubora wa hewa ya nje ya majumba

Nairobi, Septemba 2, 2021 – Theluthi moja ya nchi ulimwenguni hazina viwango vyovyote vilivyoidhinishwa kisheria kuhusu ubora wa hewa ya nje (mazingira kwa jumla) ya majumba Sheria hizo zinapokuwepo, viwango hutofautiana sana na mara nyingi haviingiani na miongozo ya Shirika la Afya Duniani (WHO). Kwa kuongezea, angalau asilimia 31 ya nchi zilizo na uwezo wa kuanzisha viwango vya ubora wa hali ya hewa bado hazijafanya hivyo. Haya ni baadhi ya matokeo muhimu ya tathmini ya kwanza kabisa ya sheria na kanuni za ubora wa hewa iliyofanywa na Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEP).

Kutunga Sheria kuhusu Ubora wa Hewa: Tathmini ya kwanza kabisa ya sheria za uchafuzi wa hewa   yazinduliwa kuelekea  Siku ya Kimataifa ya Hewa Safi ili kuwa na angaa za bluu na inachunguza sheria za kitaifa za ubora wa hewa katika Mataifa 194 na katika Muungano wa Ulaya. Kwa kuchunguza vipengele mbalimbali vya mifumo ya kisheria na taasisi, ripoti inatathmini ufanisi wake kuhakikisha kupatikana kwa viwango vya ubora wa hewa. Ripoti hiyo inahitimimika kwa kutoa vipengele muhimu vya kutumiwa kama mfano thabiti wa kushughulikia ubora wa hewa wa kuzingatiwa kwenye sheria ya kitaifa na unapendekeza kuzingatia mkataba wa kimataifa kuhusu viwango vya hali ya hewa.

Uchafuzi wa hewa umetambuliwa na WHO kama hatari kubwa zaidi kwa ubora mazingira, na asilimia 92 ya idadi ya watu ulimwenguni wanaishi maeneo yanayoshuhudia viwango hatari vya uchafuzi wa hewa, vinavyoaathiri vibaya wanawake, watoto na wazee katika nchi zenye kipato cha chini. Utafiti wa hivi karibuni unaonyesha uwezekano wa kuwa na uhusiano kati ya matokeo ya COVID-19 kwa afya na uchafuzi wa hewa.

WHO imetoa mwongozo wa kuelekeza kuhusu ubora wa hewa, lakini, kama ripoti inavyoonesha, hakuna maingiliano ya kimataifa wala mfumo maalum wa kisheria wa kuzingatia. Takribani asilimia 34 ya nchi, ubora wa hewa bado haujatungiwa sheria. Viwango vinapopatikana, ni vigumu kufanya ulinganisho: Asimimia 49 ya nchi duniani hufafanua uchafuzi wa hewa kama tishio tu la nje ya majumba. Ushughulikiaji wa viwango vya ubora wa hewa hutofautiana kwenye maeneo ya kijiografia, na zaidi ya nusu ya nchi huruhusu kutozingatiwa kwa viwango hivi.

Kwa kuongezea, jukumu la taasisi la kufikia viwango ni dhaifu kote ulimwenguni - ni asilimia 33 tu ya nchi huwajibika kufikia viwango vilivyowekwa kisheria.  Ufuatiliaji ni muhimu kufahamu iwapo viwango vinawekwa lakini haihitajiki kisheria katika asilimia 37 ya nchi.  Mwishowe, ingawa uchafuzi wa hewa hautambui mipaka, ni asilimia 31 tu ya nchi zina mifumo ya kisheria ya kushughulikia uchafuzi wa hewa unaovuka mipaka.

“Hakutakuwa na sindano ya kuzuia vifo vya mapema milioni saba vinavyosababishwa na uchafuzi wa hewa kila mwaka, idadi ambayo itaongezeka kwa zaidi ya asilimia 50 kufikia mwaka wa 2050,” alisema Inger Andersen, Mkurugenzi Mtendaji wa UNEP. Hewa tunayopumua ni haki msingi kwa umma, na serikali lazima zifanye bidii kuhakikisha kuwa ni safi na salama."

Haki ya mazingira bora, ikijumuisha hewa safi, ni muhimu ili kufikia Ajenda 2030 na Malengo ya Maendeleo Endelevu afya njema,  nishati nafuu na isiyochafua mazingira, miji endelevu, uzalishaji mwafaka na maisha kwenye ardhi (SDGs 3, 7, 11, 12, na 15). Kwenye kikao chake cha kwanza, mkutano wa 5 wa Baraza la Mazingira la UN (UNEA-5) lilitoa wito kwa Nchi Wanachama kuchukua hatua katika sekta zote kupunguza kila aina ya uchafuzi wa hewa.

Utafiti huo unaonesha kwamba "hata malengo ya kitaifa ya kupendeza ya ubora wa hewa yanapaswa kuungwa mkono na mifumo madhubuti ya taasisi, uwezo wa utekelezaji na sheria zilizoratibiwa vizuri, ikiwa zitafaulu," anasema Profesa Eloise Scotford, mwandishi mwenza wa ripoti hiyo.

Ripoti hiyo inatoa wito kwa nchi nyingi kupitisha sheria dhabiti za ubora wa hewa, ikijumuisha kuweka viwango vya juu vya sheria ya uchafuzi wa hewa ndani na nje ya majumba, kuboresha mifumo ya kisheria ya kufuatilia ubora wa hewa, kukuza uwazi, kuimarisha mifumo ya utekelezaji mno, na kuboresha uratibu wa sera na sheria za kitaifa na kimataifa za uchafuzi wa hewa.

Kufuatia tathmini hiyo, mwongozo wa vitendo tayari unaundwa na UNEP chini ya Programu ya Sheria ya Mazingira ya Montevideo ili kuimarisha msaada wake kwa nchi kushughulikia tatizo la uchafuzi wa hewa. Msaada wa kiufundi wa moja kwa moja kwa nchi, ikijumuisha maendeleo na utekelezaji wa mifumo ya kisheria ya uchafuzi wa hewa, pia inapangwa, na kujengea uwezo wadau, ikijumuisha majaji, waendesha mashtaka na maafisa wengine wa utekelezaji wa sheria.

 

MAKALA KWA WAHARIRI

Kuhusu Siku ya Kimataifa ya Hewa Safi ili kuwa na anga za bluu

Kusisitiza umuhimu wa kufanya juhudi zaidi za kuboresha ubora wa hewa, ikijumuisha kupunguza uchafuzi wa hewa, kutunza afya ya binadamu; ni kukiri kuwa kuboresha ubora wa hewa kunaweza kusaidia kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na kwamba juhudi za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi zinaweza kuboresha hali ya hewa; Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa liliamua  kuteua tarehe 7 Septemba Siku ya Kimataifa ya Hewa Safi ili kuwa na anga za bluu.

Kuhusu Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEP)

UNEP ni mhamasishaji mkubwa wa masuala ya mazingira ulimwenguni. Hutoa uongozi na kuhimiza ushirikiano katika utunzaji wa mazingira kupitia kwa kuvutia, kuelimisha na kuwezesha mataifa na watu kuimarisha maisha yao bila kuhatarisha yale ya vizazi vijavyo.     

Kwa maelezo zaidi, tafadhali wasiliana na:

Keisha Rukikaire, Msimamizi wa Habari na Vyombo vya Habari, Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa