30 Oct 2019 Tukio Kutumia mazingira kushughulikia tabianchi

Kutunza mashamba kutumia njia za kiasili kumezalia wakulima nchini Kenya matunda

"Kila mara uliza watu kile wanachohitaji, sikiliza maoni yao na uwashirikishe. Hii ndiyo tu njia ya pekee ya kuwafanya wajihisi kuwa sehemu ya mradi na kuufanya ufaulu," anasema Ivan Kiptui, Afisa wa mradi wa World Vision katika Kaunti ya Baringo nchini Kenya.

Kazi yake ni kuwafundisha wakulima kutunza mashamba yao kwa kutumia njia za  kiasili, zinazowawezesha kutunza mashamba yao kwa njia zinazohifadhi au kuboresha ekolojia. Wao hutumia elimu ya kiasili na mbinu za kisasa zinazotumika kutegemea aina ya mashamba.

Nancy Kemboi, mama wa watoto tano, amekuwa mkulima katika maisha yake yote. Ana ng'ombe 17 na kuku 20 na ishirini na anaishi katika eneo linalopokea mvua kidogo. Kabla ya hapo, angekata miti yote shambani mwake bila kung'amua umuhimu wa miti ya kiasili, na kusubiri ili nyasi iote yeyenye ili mifugo wake wapate chakula. Wangekuwa na chakula cha kutosha hadi msimu wa kiangazi halafu wakose chakula. Ili kupata pesa za kununua nyasi, wangeanza kuharibu misitu ili kupata makaa na kuni ili kujipatia hela kwa haraka.

Lakini tangu mwaka wa 2015, Kemboi alipojifunza kuhusu kutunza mashamba kwa kutumia njia za kiasili, anaelewa kuwa idadi ya watu na ya mifugo inapoendelea kuongezeka, kuna umuhimu ya kuwa wapandaji wa mimia na wafugaji kwa wakati mmoja, kupanda mimea kutumia mbinu mwafaka zisizohatarisha ekolojia.

Yeye kwa sasa hupanda nyasi na kuhifadhi mahali ambapo maji hayafikii na kuziozesha. Huhifadhi hapo hadi wakati wa kiangazi na huhitaji kufanya hivyo ili kuwa na chakula kwa mifugo wake. Siku hizi, yeye huacha miti ya kiasili shambani mwake kwa sababu huwezesha nyasi kumea vizuri kutokana na kivuli na uwezo wake wa kuhifadhi unyevu. Yeye huifadhi miti ya kiasili na lengo moja:  kupata majani kwa mifugo wake (maganda yana virutubishi vingi), kupata kuni, kupata dawa, miti mingine huvutia nyuki na kwa jumla hustahimili kiangazi na mchwa. Yeye huweka matawi ya miti na miba kwa ardhi kuifunika ili iwe na unyevunyevu. Miti asiyoihitaji inapomea, huiondoa na kuitumia kuweka ua kuzunguka  shamba lake. Ile anayoamua kutokata, yeye hupogoa matawi vizuri kwa sababu ijapokuwa miti ya kiasili hukua polepole ikilinganishwa na ya kigeni, ikipogolewa vizuri hukua kwa kasi. Pia, yeye hujaribu kukuza na kutunza  vichaka na miti kwa sababu ni rahisi kuliko kupanda miche.

Kemboi pia amechimba mitaro shambani mwake ili kupunguza mmomonyoko wa udongo na kuhifadhi maji. Pia anapanda mimea kwa kutumia njia bora; anapanda viazi, kabichi, nyanya na aina nyingine ya mboga katikati ya mahindi na miti ya matunda. Miti ya matunda huvutia popo na ndege na kuongeza bayoanuai ya mifumo ya ekolojia.

image

Kwa miaka minne iliyopita, Kemboi amekuwa mkulima wa kupigiwa mfano katika mfumo wa kutunza mashamba kutumia njia za kiasili na ametoa mafunzo kwa wakulima wengine kumi. "Maisha yangu yameboreka sana," anasema. "Kwa sababu nina vyanzo vingi vya kupata pesa, kutoka kwa mimea yangu ya mahindi, mboga zangu na ufugaji wa nyuki, nilifanikiwa kununua aina bora ya ng'ombe wanaotoa maziwa mengi. Kwa hivyo, mimi hupata fedha zaidi."

Mradi wa kutunza mashamba kutumia njia za kiasili  pia hutoa mafunzo kwa vijana walio na matatizo ili kuwapa fursa ya kurudi mashambani. "Wao hushiriki kwa hiari kwa kuzingatia utaratibu uliowekwa na wadau mbalimbali na sheria zilizowekwa  kwa msaada wa Wizara ya Mazingira na Misitu kama sehemu ya mradi wa UN-REDD unaolenga kusaidia Kenya kupitia kwa Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa," anasema Judy Ndichu, Mratibu wa Kiufundi wa 'Forest Carbon Partnership Facility' nchini Kenya. "Unatoa fursa kwa jamii kushiriki wakati wa mchakato wa kufanya maamuzi kuhusu miradi inayohusu misitu wanayoitegemea ili kuishi."

"Mbali na kukabiliana na gesi ya ukaa, na hivyo kuchangia malengo ya kimataifa ya kuipunguza, kuimarisha mazingira huwezesha kuwa na chakula cha kutosha, kuongeza ustahimilivu na kuhifadhi bayoanuai. Eneo la mradi likiongezwa, manufaa yatapatikana kutokana na mifumo ya ekolojia kuimarika na watu kukua vizuri," anasema Gabriel Labbate, Kinara wa Kikosi cha Kimataifa cha Mradi wa  UN-REDD.

Mmoja wa wakulima aliyepata mafunzo kutoka kwa Kemboi, David Korrir, anasema: "Shamba hili ndlo dhahabu yangu. Nimewekeza kwa upanzi wa miti, kupanda mboga kati ya aina mbalimbali ya miti ya matunda kama vile miembe, mipaipai ili niweze kuvuna kitu kila wakati na kuepukana na njaa. Vizazi vijavyo vitanufaika kutokana na shamba langu na miti ya kiasili iliyomo iliyofanya ndege na nyuki kurudi."

image

Mifumo bora ya ekolojia ni muhimu kwa maisha ya binadamu. Kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, kuhakikisha kwamba kuna chakula  na maji ya kutosha, kukuza uchumi na kuhifadhi bayoanuai, yote haya hutegemea mifumo bora ya ekolojia inayofanya kazi vizuri. El Salvador ilitangulia na nchi zaidi ya 70 kutoka maeneo mbalimbali zikafata nyayo, Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa ulitangaza karne ya  2021 hadi 2030 kuwa Karne ya Uboreshaji wa Mifumo ya Ekolojia . Hali hii inafanya uboreshaji wa mifumo ya ekolojia kuwa suhuhisho mwafaka linalozingatia njia za kiasili kutatua masuala mengi nyeti ya kitaifa.