Picha na Reuters/ Eric Lafforgue
14 Jun 2022 Tukio Kutumia mazingira kushughulikia tabianchi

Somalia attempts to revive lands blighted by deforestation

Picha na Reuters/ Eric Lafforgue

Wakati ambapo mkulima Mohamed Ibrahim Aden hashughulikii mashamba yake binafsi, mara nyingi unaweza kumpata akinyuzia miche maji kwenye bustani ndogo ya miche inayomilikiwa na jamii katika kijiji cha Gobweyn nchini Somalia.

Migunga inayopandwa na Aden itatumiwa kupandwa katika eneo hili kame nchini Somalia. Eneo linalopatikana mita chache kutoka Bahari Hindi, ni sehemu ya juhudi kabambe za kupanda miti kwa ardhi iliyoharibiwa na ukataji wa miti. 

"Nitatunza miche ya miti vizuri," alisema Aden mwenye umri wa miaka 64, ambaye aliiita urithi kwa watoto wake na wajukuu wake.

Mradi huo wa bustani ya miche, unaoungwa mkono na mashirika kadhaa ya Umoja wa Mataifa, unalenga kusaidia kurejesha misitu kusini mwa Somalia, ambayo imeharibiwa kwa miaka mingi kupitia ukataji haramu. Kupungua kwa miti katika eneo hilo kumeongeza mmomonyoko wa udongo na kupunguzia ardhi uwezo wake wa kuhifadhi maji, hali ya kutisha kwa nchi inayoshuhudia ukame mbaya zaidi katika kipindi cha miaka 40. 

"Kuboresha mazingira ni muhimu sana sio tu kwa ubora wa udongo, lakini pia ili kupunguza mvutano unaohusu kushindania malighafi na kupunguza watu kuhama makwao kutokana na mafuriko na ukame," alisema Christophe Hodder, Mshauri wa Somalia wa Kitengo cha Usalama wa Hali ya Hewa na Mazingira cha Umoja wa Mataifa. 

Kukata miti

Migunga, miti ya mbao ngumu inayokua polepole, ni muhimu kwa hali ya hewa ya joto na ukame nchini Somalia. Huimarisha rutuba ya udongo kwa kuhifadhi maji, kuweka nitrojeni ambayo ni mbolea muhimu, na kupunguza kukatikakatika kwa udongo na mmomonyoko wa udongo wakati wa msimu wa mvua. 

Hata hivyo, biashara haramu inayoshamiri ya makaa  - yanayopatikana kwa kuchoma mbao- inaangamiza miti hii. Utafiti wa hivi majuzi uliweka kiwango cha kupungua kwa kila mwaka cha spishi moja iliyo hatarini, Acacia bussei, kuwa juu kwa kiwango cha asilimia 5. Maeneo yaliyoathirika zaidi ni Jubaland, Sool Sanaag na Buhoodle.

A man stands beside a carcass of a goat
Ukame mbaya zaidi kuwahi kushuhudiwa nchini Somalia katika kipindi cha miaka 40 umeharibu ardhi ambayo tayari inakabiliwa na ukataji miti na uchungaji mifugo kupita kiasi.  Picha na Reuters/Feisal Omar

Makaa ni chanzo kikuu cha nishati nchini Somalia, ambako ni watu wachache tu wanapata umeme.  Pia imesafirishwa kwa nchi kama vile Saudia, Yemen, na Falme za Kiarabu. 

Ingawa Somalia ilipiga marufuku mauzo ya makaa na kuni nje ya nchi katika mwaka wa 1969, imekuwa vigumu kutekeleza. Uzalishaji haramu wa makaa usio na kikomo uliongezeka baada ya Serikali ya Somalia kusambaratika katika mwaka wa 1991. 

Kama Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa lilivyoonyesha, ukuaji wa sekta ya makaa nchini Somalia umekuwa chanzo cha mzozo. Mvutano umepamba moto kati ya wakata kuni, wanamgambo wanaojihusisha na biashara ya makaa na jamii za vijijini, ambazo maisha yao yanatishiwa na ukataji wa miti. 

Katika mwaka wa 2012, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilipitisha Azimio 2036, ambalo lilipiga marufuku usafirishaji na uagizaji wa makaa nchini Somalia.

Hii ilifuatiwa mwaka wa 2016 na uzinduzi wa Mpango Endelevu wa Kupunguza Makaa na Maisha Mbadala (PROSCAL), ushirikiano kati ya Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa, Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa, na Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa.

Mpango huo umesaidia maafisa wa Somalia kutekeleza marufuku ya makaa, kuunga mkono ukuzaji wa vyanzo vya nishati mbadala, kuboresha ardhi iliyoharibiwa na kusaidia wakazi wa eneo hilo kupata kazi endelevu zaidi.

"Programu ya PROSCAL imeimarisha kiwango cha uelewa, kwa kuelimisha umma kuhusu athari za uzalishaji haramu wa makaa na umuhimu wa kuacha au kupunguza uzalishaji huo," alisema Hodder.  Pia imesaidia kuchochea matumizi ya gesi ya petroli kama nishati na kupunguza hitaji la makaa, alisema.

 Changamoto ya tabianchi

Mabadiliko ya tabianchi huongeza, umaratokezi na makali ya ukame hali inayotarajiwa kukumba Pembe ya Afrika. Wataalamu wanahofia kuwa huenda ukasambaratisha mifumo ya ekolojia ambayo tayari ni dhaifu - ikiwa ni pamoja na ile iliyoathiriwa na ulishaji wa mifugo kupita kiasi, kulima kupita kiasi na ukataji wa miti - na kuwaacha watu hatarini kukabaliwa na baa la njaa. Nchi hiyo kwa sasa inakabiliwa na ukame mbaya zaidi kuwahi kutokea katika miongo kadhaa. Zaidi ya mifugo milioni saba wamekufa na mamilioni ya watu wanatishiwa na njaa.

Wakati huo huo, Somalia haiwezi kutegemea chakula cha msaada kufidia udongo usio na rutuba, alisema Hodder. Mwaka jana, asilimia 53 ya chakula ambacho Shirika la Chakula Duniani lilipokea nchini Somalia kilitoka katika nchi inayokumbwa na vita vya Ukraine na bei ya vyakula duniani inazidi kupanda.

A family stands beside a canvas hut.
Mradi unaoungwa mkono na Umoja wa Mataifa unasaidia jamii za Kisomali kutafuta njia mbadala za uzalishaji wa makaa, chanzo ambalo lkikuu cha ukataji wa miti. Picha na Reuters/Zohra Bensemra

Programu ya PROSCAL umeundwa ili kusaidia jamii kustahimili vitisho kama hivyo, kwa upande mmoja kupitia upandaji wa miti. Bustani mbili za miche zimeanzishwa Gobweyn na kijiji cha Yontoy, katika jitihada za kusaidia kuboresha ardhi na kutoa maisha endelevu kwa wanakijiji.

"Ninawahimiza watu katika kijiji changu kupanda miti ili waweze kuitumia katika miaka ijayo," Deeqa Abdi Osman mwenye umri wa miaka 40 alisema. 

Anaishi na watoto wake watatu huko Yontoy.  Mwanachama wa kamati ya eneo la bustani la miti, anashukuru kwa msaada kutoka kwa Umoja wa Mataifa na Muungano wa Ulaya, ambao kwa kiasi fulani wanafadhili mradi huo.   

"Mradi umeimarisha uwezo wetu na maarifa yetu kuhusiana na usimamizi wa maliaghafi, usimamizi wa vikundi na usimamizi wa fedha, hali itakayotusababashia manufaa ya kudumu kama watu binafsi na kama jamii ya Yontoy," alisema.

Wakati uo huo, mradi huo umetoa vyanzo vya nishati vinavyojali mazingira, kama vile majiko yasiyotumia fueli nyingi na paneli za jua.  Mwishoni mwa mwaka wa 2021, zaidi ya familia 12,000 katika eneo la Programu tayari zilikuwa zimeacha kutumia makaa yanayopatikana katika eneo na kuanza kutumia gesi ya petroli kupikia.  

Awamu ya kwanza ya programu ya PROSCAL itakamilika Desemba mwaka wa 2022.  Mafanikio yake yatahitaji kuigwa na kuimarishwa, nchini Somalia na kwingineko, wakati Umoja wa Mataifa unapoanza Muongo wake wa Kuboresha Mifumo ya Ekolojia 2021-2030, alisema Hodder. 

Mwaka jana, Serikali ya Somalia ilianzisha majadiliano na mashirika matatu ya Umoja wa Mataifa ili kueneza programu ya PROSCAL kote nchini. Awamu inayofuata inatarajiwa kusisitiza kipengele cha kisiasa na usalama cha uzalishaji wa makaa usio endelevu, ikionyesha uhusiano kati ya mazingira salama, kupoteza makao na mizozo. 

Unaweza kusoma zaidi kuhusu kazi za UNEP ya kukabiliana na ukataji wa miti na kukuza mifumo dhabiti ya ekolojia kote duniani hapa.