01 Sep 2020 Toleo la habari Kushughulikia Mazingira

Hatua za kuimarisha hali ya hewa kwa mifumo ya chakula zinaweza kupunguza uchafuzi duniani kwa asilimia 20 inavyotakikana kabla ya mwaka wa…

September 1, 2020 - Watunga sera wanaweza kuimarisha uwezekano wa kufikia malengo ya hali ya hewa na kudhibiti ongezeko la joto duniani kuwa nyuzijoto 1.5 kupitia ahadi dhahiri mno na kwa kubadilisha mifumo ya kitaifa ya chakula. Kuimarisha Ahadi Zilizowekwa na Taifa (NDCs) za Mifumo ya Chakula, ripoti mpya iliyochapishwa leo na WWF, Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEP), EAT na Climate Focus, inaonyesha kuwa nchi zinapitwa na fursa muhimu za kupunguza uzalishaji wa gesi ya ukaa na kuanisha njia 16 ambazo watunga sera wanaweza kutumia ili kuchukua hatua zaidi, tangu shambani hadi mezani.

Kwa sasa, lishe, upoteaji wa chakula na uharabifu wa chakula hupuuzwa mno, lakini kwa kuongeza kwenye mikakati ya kitaifa ya hali za hewa, waunda sera wanaweza kuimarisha na kuboresha mifumo ya chakula, kwa kiwango kikubwa cha  asilimia 25. Chini ya Mkataba wa Paris wa mwaka wa 2015, nchi zinatarajiwa kutoa upya ahadi zake za NDCs kila baada ya miaka mitano. Mwaka huu, kwa hivyo, watunga sera wana fursa ya kutoa suluhu kwa mifumo ya chakula na kuweka malengo mwafaka zaidi na kuchukua hatua za kupunguza uzalishaji wa gesi ya ukaa na kwa hivyo, kuimarisha mifumo ya bayoanuai, utoshelezaji wa chakula na afya ya umma.

Mifumo ya Chakula – inayojumuisha vipengele vyote na shughuli zote kuhusiana na uzalishaji, utengenezaji, usambasaji, uandaaji na ulaji wa chakula –unachangia ongezeko la asilimia 37 ya uzalishaji wa gesi zote za ukaa; kuendelea jinsi hali ilivyo kama kawaida tu kutatumia bajeti yote inayowezesha uzalishaji wa gesi chafu usiozidi nyuzijoto 1.5 katika sekta zote. Ijapokuwa asilimia 89 ya NDCs zote hutaja kilimo, malengo ya kupunguza uzalishaji wa gesi chafu kutokana na kilimo hujumuishwa tu zaidi kwenye matumizi mapana ya ardhi. La muhimu, juhudi zingine katika mifumo ya chakula, kama vile kupunguza upoteaji na uharibifu wa chakula, au kuanza kutumia lishe bora zaidi, mara nyingi hupuuziliwa mbali, ijapokuwa ni fursa ya kupunguza uzalishaji wa gesi ya ukaa kwa gigatani 12.5 za kaboniksidi kila mwaka, - kiasi sawa na cha uzalishaji wa magari madogo bilioni 2.7 yanaposafiri.

"Ahadi kabambe, zinazowekewa mda maalum na zinazoweza kupimika za kubadilisha mifumo ya chakula zinahitajika ili kufikia nyuzijoto 1.5 katika siku zijazo. Kutofanya hivyo ni kupuuza vyanzo vikuu vya majanga yanayotokea siku hizi kutokana na hali ya hewa. Bila kuchukua hatua kuhusiana na jinsi tunavyozalisha na kutumia chakula, hatuwezi kufikia malengo yetu ya hali ya hewa na ya bayoanuai, ambayo ni nguzo ya kuwezesha utoshelezaji wa chakula, kuzuia kuzuka kwa magonjwa na hatimaye kufikia Malengo ya Maendeleo Endelevu. Hii ndiyo sababu tunatoa wito kwa serikali kujumuisha hali ya hewa na mifumo ya chakula inayojali mazingira kwa NDCs mpya kabambe zinazotolewa huu mwaka," alisema Marco Lambertini, Mkurugenzi Mkuu wa WWF-International.

"Janga la korona limeonyesha udhaifu wa mifumo yetu ya usambasaji wa chakula, kuanzia kwa mifumo yake changamano hadi kwa athari kwa mifumo yetu ya ekolojia. Lakini pia imeonyesha kuwa mashirika ya biashara na watu wako tayari kujiimarisha baada ya korona. Janga hili linatoa fursa kwetu ya kuwaza kuhusu jinsi tanavyozalisha na kutumia chakula. Kwa mfano, kubadili utumiaji wa chakula kwa kupunguza uharibifu mara dufu na kula vyakula vinavyotokana na mimea zaidi, ni njia mwafaka ya kukabiliana na hali ya hewa kwa manufaa yetu. Ni jukumu letu kuchukua fursa hii na kubuni mifumo ya kudumu ya chakula kama nguzo muhimu ya kupunguza uchafuzi." alisema Inger Andersen, Mkurugenzi Mtendaji wa UNEP.

Njia 16 ambazo zimeorodheshwa katika ripoti hiyo ni pamoja na kupunguza mabadiliko katika matumizi ya ardhi na mabadiliko kwa makazi asilia, vinaweza kupunguza uzalishaji wa gesi chafu kwa gigatani 4.6 za kabonikisidi kwa mwaka. Kwa kulingalisha na kupunguza uharibifu wa chakula, unaokadiria asilimia 8 ya uzalishaji wa gesi ya ukaa (GHG) hatua hizi zinaweza kupunguza uzalishaji wa gesi chafu kwa gigatani 4.5 za kabonikisidi kwa mwaka. Hata hivyo, ni nchi 8 tu ambazo zimetaja upoteaji wa chakula katika mikakati yake wala hakuna iliyozingatia uharibifu wa chakula. Kuimarisha njia za uzalishaji na kupunguza uzalishaji wa methani kutoka kwa mifugo, kunaweza kupunguza uzalishaji wa gesi chafu kwa gigatani 1.44 za kaboniksidi kwa mwaka, ila upunguzaji zaidi unaweza kutokea kwa kuanza kutumia lishe bora ya kudumu huku sehemu kubwa ya lishe hiyo ikitokana na mimea badala ya wanyama. Hali inayoweza kupunguza uzalishaji wa gesi chafu kwa gigatani  8 za kaboniksidi kila mwaka. Hakuna mikakati ya kitaifa inayojadili wazi lishe ya kudumu.

Ripoti hiyo inaonyesha kuwa kuna uwezekano mdogo kwa nchi zilizoendelea ikilinganishwa na nchi zinazoendelea wa kuweka hatua zilizo wazi za kukabiliana na hali ya hewa katika mikakati yake iliopo. Lakini, hatua wazi za kupunguza uzalishaji wa gesi chafu kwenye mifumo ya chakula katika nchi zinazoendelea bado duni. Katika mwezi wa Agosti mwaka wa 2020 NDC 15 zilizosasishwa na kupitiwa upya zilipokelewa na ijapokuwa baadhi inazungumzia kilimo, hatua bado hazijachukuliwa. Viashiria vya mwanzo vinaonyesha kuwa matumizi ya chakula cha kudumu na upoteaji na uharibufu wa chakula ni mambo yanayoendelea kupuuzwa wakati wa mchakato wa kupitia NDC. Kwa masasisho yaliyopokelewa baada ya kupitiwa upya hakuna yanayotaja mambo haya kwenye masuluhisho au kwenye sera na mikakati.

"Mifumo ya chakula hupuuzwa ila ni muhimu katika kukabiliana na uharibifu na ina manufaa mengi ya kudumu katika mchakato wa maendeleo. Kukomesha matumizi ya nyama zaidi, kuboresha maghala na kupunguza uharibifu wa chakula ni mzuri kwa afya yetu na huimarisha utoshelezaji wa chakula. Kwa kuorodhesha na kutoa mifano dhabiti ya shughuli na malengo, ripoti hii inatoa ushauri kwa watunga sera kujumuisha mifumo ya chakula katika mikakati yake ya kitaifa,” alisema Charlotte Streck, Mwanzilishi Mwenza na Mkurugenzi wa, Climate Focus.

"Kushughulikia chakula sio tu muhimu ili kufikia Ajenda ya mwaka wa 2020, lakini ni muhimu kama mabadiliko katika matumizi ya nishati ili kuweza kufikia Makubaliano ya Mkataba wa Paris. Kuanza kufanya uzalishaji kwa njia zilizoboreshwa, zinazokabiliana na ukaa na kutumia lishe yenye afya, hasa kutokana na mimea inayopatikana kwa bei nafuu na kwa urahisi, ikiwa ni pamoja na kupunguza uharibifu na upoteaji wa chakula, ni mambo muhimu yanayopaswa kujumuishwa katika NDC na kujumuishwa katika mikakati ya hali ya hewa kikamilifu. Tunapoingia katika Muongo wa Kuchukua Hatua, tuufanye muongo wa kuwezesha kuwa na chakula cha afya, cha kudumu na kinachopatikana kwa watu wote bila upendeleo katika siku zijazo,” alisema Dkt. Gunhild Stordalen, Mwanzilishi na Mwenyekiti Mkuu wa EAT.

Pamoja na kuimarisha NDC zake, nchi zina fursa zingine zaidi za kupunguza uzalishaji wa gesi chafu na kutunza mazingira kupitia mifumo ya chakula. Katika mwaka wa 2021, katika muktadha wa Kongamano la Nchi Wanachama (COP 15) wa Mkataba wa Bayoanuai ya Kibayolojia wa Umoja wa Mataifa, viongozi duniani wanaweza kukubaliana kuweka malengo mapya ya zazingira na watu, ili kusitisha na kukabiliana na uharibifu wa bayoanuai. Kwa kuongezea, mkutano wa kwanza kuwahi kutokea, Mkutano Mkuu wa UN wa Mifumo ya Chakula utatendeka mwaka wa 2021; alivyosema Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres alipokuwa anazindua Mkutano Mkuu, "kubadilisha mifumo ya chakula ni muhimu ili kufikia Malengo ya Maendeleo Endelevu".

 

MAKALA KWA WAHARIRI

Kuhusu WWF

WWF ni shirika la uhifadhi linalojitegemea, lililo na wafuasi zaidi ya milioni 30 kote duniani na linapatikana katika nchi karibu 100. Lengo letu ni kusitisha uharibifu wa malighafi katika mazingira na kujenga mustakabali ambao kila mtu anaishi vyema na mazingira, kwa kuhifadhi mifumo ya bayoanuai ya kibayolojia, kuhakikisha kuwa malighafi zinatumiwa kwa njia endelevu na zinaweza kutumiwa tena, na kupunguza uchafuzi  na matumizi mabaya ya bidhaa. Tembelea panda.org/news kufahamu kuhusu taarifa za hivi punde na rasilimali za vyombo vya habari; tufuate kwenye Twitter @WWF_media

Kuhusu Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEP)

UNEP ni mhamasishaji mkubwa wa masuala ya mazingira duniani. Hutoa uongozi na kuhimiza ushirikiano katika utunzaji wa mazingira kupitia kwa kuvutia, kuelimisha na kuwezesha mataifa na watu kuimarisha maisha yao bila kuhatarisha yale ya vizazi vijavyo.

Kuhusu Climate Focus

Climate Focus ni kampuni ya kwanza kutoa ushauri wa kimataifa na kufanya utafiti na kuandika ripoti zinazotoa ushauri kuhusu sera za kimataifa za hali ya hewa kwa sekta ya umma na sekta ya binafsi duniani. Huwa tunasaidia wateja wetu kuandaa na kutekeleza sera za kimataifa na za ndani ya nchi kuhusiana na hali ya hewa, kupata ufadhili wa kugharamia hali ya hewa, na kushirikiana na wateja wapya kuunda mbinu na mikakati kuhusu hali ya hewa. Sisi hushughulikia mno ardhi, utunzaji wa misitu ya tropiki na kilimo endelevu. 

Climate Focus ilianzishwa mwaka wa 2004 na ina ofisi mjini Amsterdam, Rotterdam, Berlin, Washington DC, na Bogotá. Kikosi chetu hushirikiana na wataalamu ndani ya nchi na wa kimataifa.

Kuhusu EAT

EAT ni shirika la kimataifa lisilo la biashara lililoanzishwa na Wakfu wa Stordalen, Kituo cha Stockholm Resilience Centre na Wellcome Trust, na hufanya kazi kuhakikisha kuna mabadiliko katika mfumo wa chakula duniani. Dira yetu ni kuwa na mfumo endelevu wa kimataifa wa chakula ili kuwa na watu wenye afya na sayari bora - bila kumubagua yeyote. Shirika hili hujumuika na kushirikiana na wabia kufadhili sayansi, sera, mashirika ya biashara na mashirika ya uraia ili kuleta mabadiliko kwenye mifumo ya chakula duniani kupitia sayansi yenye hakika, kukabiliana na usumbufu na kutafuta wafadhili wapya.

Kwa taarifa zaidi, tafadhali wasiliana na:

Peter McFeely, Msimamizi wa mawasiliano ya kimataifa, Chakula, WWF
Keishamaza Rukikaire, Msimamizi wa Habari na Vyombo vya Habari, UNEP