Picht: Darya Kuznetsova / UNEP
13 Dec 2022 Toleo la habari Kutumia mazingira kushughulikia tabianchi

UN yatuza miradi 10 chipukizi inayoboresha dunia asilia

Picht: Darya Kuznetsova / UNEP
  • Juhudi kuanzia Amerika ya Kati hadi Asia Mashariki zatuzwa kama Miradi Mikuu ya Uboreshaji wa Mifumo ya Ekolojia Duniani 
  • Miradi hiyo sasa imetimiza masharti ya kukuzwa, kupokea ushauri au ufadhili kutoka kwa Umoja wa Mataifa
  • Miradi hiyo ilizinduliwa katika tamasha kubwa lililowashirikisha Dkt. Jane Goodall, Jason Momoa, Li Bingbing, Filipe Toledo, Frida Amani, Edward Norton, Ellie Goulding na wengineo   

Montreal, Desemba 13, 2022 - Umoja wa Mataifa umetuza juhudi 10 za msingi kutoka kote duniani kutokana na wajibu wao wa kuboresha dunia asilia.

Miradi iliyoshinda ilizinduliwa katika Kongamano la Umoja wa Mataifa la Bayoanuai (COP15) mjini Montreal na tamasha maalum la mtandaoni lililowashirikisha waigizaji Jason Momoa na Edward Norton, Dkt. Jane Goodall, mpanda milima mkuu Nirmal Purja, mwimbaji Ellie Goulding, bendi ya Bastille kutoka Uingereza, mtu mashuhuri nchini China Li. Bingbing, Mkurugenzi Mtendaji wa UNEP Inger Andersen, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa FAO Maria Helena Semedo na mwanauchumi wa Uingereza Sir Partha Dasgupta, miongoni mwa wengineo. Tamasha hilo liliandaliwa na Mtaalamu wa Kitaifa wa Masuala ya Jiographia kutoka India na mtayarishaji filamu ya wanyamapori Malaika Vaz. 

Miradi hiyo ilitangazwa kuwa Miradi Mikuu ya Kuboresha Mifumo ya Ekolojia Duniani na imetimiza masharti ya kukuzwa, kupokea ushauri au ufadhili kutoka kwa Umoja wa Mataifa. Walichaguliwa chini ya Muongo wa Umoja wa Mataifa wa Kuboresha Mifumo ya Ekolojia, vuguvugu la kimataifa linaloendeshwa na Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEP) na Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO). Unalenga kuzuia na kukabiliana na uharibifu wa maeneo ya kiasili katika sayari nzima.  

Kwa ujumla, miradi hiyo 10 inalenga kurejesha misitu kwa zaidi ya hekta milioni 68 - eneo kubwa kuliko Myanmar, Ufaransa au Somalia - na kubuni nafasi za kazi takribani milioni 15.   

Wakati wa uzinduzi wa Miradi Mikuu ya Kuboresha Mifumo ya Ekolojia Duniani, Muongo wa Umoja wa Mataifa unalenga kutuza mifano bora ya kuigwa ya uboreshaji wa mifumo ya ekolojia kwa kiwango kikubwa na kwa kipindi kirefu, kwa kuzingatia Kanuni 10 za Uboreshaji za Muongo wa Umoja wa Mataifa wa Kuboresha Mifumo ya Ekolojia.

Muongo wa Umoja wa Mataifa unatambua kuna muda unaohitajika kwa juhudi za kuboresha mifumo ya ekolojia kuzalisha matunda. Hadi kufikia mwaka wa 2030, wito utatolewa mara kwa mara wa Miradi Mikuu ya Kuboresha Mifumo ya Ekolojia Duniani kuzinduliwa. Kwa kutarajia kuongezeka kwa ufadhili kwa Mfuko wa Wabia Mbalimbali wa Umoja wa Mataifa (MPTF), ufadhili zaidi utazingatiwa, ikijumuisha miradi ya uboreshaji wa mifumo ya ekolojia kutoka Pakistan, Peru, na mradi unaolenga Somalia na nchi nyingine zilizoathiriwa na ukame.

 

Mkurugenzi Mtendaji wa UNEP Inger Andersen: "Kubadilisha uhusiano wetu na mazingira ni nguzo ya kukabiliana na changamoto za aina tatu duniani za mabadiliko ya tabianchi, uharibifu wa mazingira na wa bayoanuai, na uchafuzi na taka. Miradi 10 Mikuu Chupukuzi ya Kuboresha Mifumo ya Ekolojia inaonyesha kuwa tukiwa na utashi wa kisiasa, sayansi, na ushirikiano wa kimataifa, tunaweza kufikia malengo ya Muongo wa Umoja ya Kuboresha Mifumo ya Ekolojia na kubuni mustakabali endelevu zaidi kwa manufaa ya sayari na kwetu sisi tunayoiita nyumbani.”   

Qu Dongyu, Mkurugenzi Mkuu wa FAO, alisema: "FAO, pamoja na UNEP, kama wasimamizi wenza wa Muongo wa Umoja wa Mataifa wa Kuboresha Mifumo ya Ekolojia, wanafuraha kutuza miradi 10 kabambe inaayotia matumaini ya uboreshaji wa mifumo ya ekolojia kama Miradi Mikuu ya Kuboresha Mifumo ya Ekolojia Duniani katika mwaka wa 2022. Kwa kuchochewa na miradi hii mikuu, tunaweza kujifunza kuboresha mifumo yetu ya ekolojia ili kuzalisha vyema, kuwa na lishe bora, mazingira bora na maisha bora kwa wote, bila kumwacha yeyote nyuma." 

Miradi 10 Mikuu Chupukuzi ya Kuboresha Mifumo ya Ekolojia Duniani ni:

Muungano wa Kutunza Misitu ya Atlantiki Iliyo katika Nchi Tatu

Kuna wakati Misitu ya Atlantiki ilienea nchini Brazil, Paraguay na Argentina. Lakini imepunguzwa na kuwa vijisehemusehemu kutokana na karne nyingi za ukataji miti, upanuzi wa eneo la kilimo na ujenzi wa majiji.  

Mamia ya mashirika yanafanya juhudi zitakazodumu miongo kadhaa za kulinda na kurejesha msitu katika nchi zote tatu. Miradi yao inabuni maeneo ya wanyamapori hususan kwa viumbe walio hatarini kuangamia, kama vile jagua na simba aina ya tamarin, kuhakikisha watu na mazingira wanapata maji, kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na kujenga uwezo wa kuyahimili, na kubuni maelfu ya nafasi za kazi.    

Angalau hekta 700,000 tayari zimerejeshwa kuwa na msitu huku lengo likiwa kufikia hekta milioni 1 kufikia mwaka wa 2030 na hekta milioni 15 kufikia mwaka wa 2050.

Kuboresha Ekolojia ya Maeneo ya Bahari Nchini Abu Dhabi 

 Kulinda nguva, ambao idadi yao ni ya pili kwa ukubwa duniani ni lengo la juhudi katika Miliki za Falme za nchi za Kiarabu za kurejesha nyasi za maeneo ya bahari – chakula kinachopendelewa na nguva – pamoja na miamba ya matumbawe na mikoko kwenye pwani ya Ghuba. 

Mradi huu kwenye eneo la Abu Dhabi utaboresha hali ya mimea na wanyama wengine wengi, ikijumuisha aina nne za kasa na aina tatu za pomboo. Jamii za wenyeji zitafaidika kutokana na kurejea kwa angalau spishi 500 za samaki, pamoja na kutoa fursa nyingi zaidi kwa utalii wa mazingira.    

Abu Dhabi inataka kuhakikisha kuwa mifumo yake ya ekolojia ya maeneo ya pwani inaweza kustahilili ongezeko la joto duniani na maendeleo ya haraka katika maeneo ya pwani katika kile ambacho tayari ni mojawapo ya bahari zilizo na kiwango cha juu zaidi cha joto duniani.   

Takriban hekta 7,500 za mifumo ya ekolojia ya maeneo ya pwani zimeboreshwa huku hekta nyingine 4,500 zikiendelea kuboreshwa hadi mwaka wa 2030.

Ukuta Mkubwa wa Kijani kwa Uboreshaji wa Mifumo ya Ekolojia na kwa Amani 

Ukuta Mkubwa wa Kijani ni juhudi kabambe za kurejesha ekolojia ya maeneo ya savana, nyanda na mashamba barani Afrika ili kusaidia familia na bayoanuai kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na kuzuia kuenea kwa jangwa kuendelea kutishia zaidi jamii ambazo tayari ziko hatarini.     

Mradi uliozinduliwa na Muungano wa Afrika katika mwaka wa 2007, unalenga kubadilisha maisha ya mamilioni ya watu katika eneo la Sahel kwa kuunda ukanda wa mandhari ya kijani yatakayofaidi nchi 11.    

Dhamira ya Ukuta Mkubwa wa Kijani kufikia mwaka wa 2030 ni kupanda miti kakita eneo la hekta milioni 100, kuteka tani milioni 250 za hewa ya ukaa na kubuni nafasi milioni 10 za kazi.

Ijapokuwa Ukuta Mkuu wa Kijani unalenga ardhi iliyoharibika kote barani Afrika, miradi mikuu ya Muongo wa Umoja wa Mataifa itaangazia hasa Burkina Faso na Niger. 

Uboreshaji wa Mto Ganges

Kuboresha hali ya mto Ganges, mto mtakatifu wa India, ni lengo la juhudi kuu za kupunguza uchafuzi, kurejesha misitu na kunufaisha watu milioni 520 wanaoishi karibu na mto huo kwa njia mbalimbali.   

Mabadiliko ya tabianchi, ongezeko la watu, ukuaji wa viwanda na unyunyuziaji mimea maji vimeharibu mto Ganges kwenye chanzo chake cha kilomita 2,525 kutoka Himalaya hadi Ghuba ya Bengal.     

Mradi uliozinduliwa katika mwaka wa 2014, Namami Gange ni mradi unaosimamiwa na serikali unaorejesha misitu katika maeneo ya mto Ganges na kukuza kilimo endelevu. Pia ualenga kurejesha aina kuu za wanyamapori, ikijumuisha pomboo wa mtoni, kasa wa ganda laini, fisi maji, na samaki aina ya hilsa shad. 

Uwekezaji wa serikali ya India ni hadi dola bilioni 4.25 kufikia sasa. Mradi huuo unahusisha mashirika 230, huku kilomita 370 za mto zikiwa zimeboreshwa kufikia sasa. Mbali na hayo, hekta 30,000 zimepandwa miti kufikia sasa, na lengo  la kufikia hekta 135,000 kufikia mwaka wa 2030.

Mradi wa Mbalimbali za Maeneo ya Milima

Nchi za maeneo ya milima hukabiliwa na changamoto za kipekee. Mabadiliko ya tabianchi yanapelekea kuyeyuka kwa barafu, mmomonyoko wa udongo na kuhatarisha maisha ya viumbe mbalimbali – mara nyingi kuvipelekea kuwa karibu kutoweka. Maji ambayo milima hutoa kwa mashamba na kwa miji katika maeneo tambarare yasiyoinuka yanazidi kutoweza kutegemewa.    

Mradi huu ulioko Serbia, Kyrgyzstan, Uganda na Rwanda unaonyesha jinsi miradi hiyo katika maeneo matatu yanayotofautiana inavyotumia uboreshaji kufanya mifumo ya ekolojia ya maeneo ya milimani kuwa dhabiti zaidi ili kuyawezesha kusaidia wanyamapori wa kipekee na kutoa manufaa makuu kwa watu. 

Uganda na Rwanda ni makaazi kwa mojawapo ya sokwe wawili tu waliosalia wa maeneo ya milimani walio hatarini kuangamia. Kutokana na kutunza makaazi yao, idadi ya sokwe imeongezeka maradufu katika kipindi cha miaka 30 iliyopita. Nchini Kyrgyzstan, wafugaji wanasimamia maeneo ya malisho kwa njia endelevu zaidi ili kupata chakula bora kwa mifugo na mbuzi wa Asia. Chui wa maeneo ya theluji wanaongezeka polepole.  Nchini Serbia, mamlaka inapanua maeneo yaliyopandwa miti na kukuza maeneo ya kulisha mifugo katika maeneo mawili yaliohifadhiwa. Dubu wa kahawia wamerejea misituni, ambapo uboreshaji pia unasaidia mifumo ya ekolojia kuimarika kutokana na mioto misituni.

Mradi wa Kuboresha Mifumo ya Ekolojia katika Nchi za Visiwa Vidogo

Juhudi zinaangazia nchi tatu zinazoendelea za visiwa vidogo – Vanuatu, St Lucia na Komoro – miradi hii mikuu   inakuza urejeshaji wa mifumo ya kipekee ya ekolojia na kuwezesha ukuaji wa uchumi unaotegemea bahari ili kusaidia jamii za visiwa kujinasua kutokana na athari za janga la COVID-19.    

Malengo yake ni kupunguza shinikizo kwenye miamba ya matumbawe, ambayo yanaweza kuharibiwa na dhoruba, ili akiba ya samaki iweze kurudi kuwepo. Mifumo ya ekolojia inayoboreshwa pia inajumuisha mwani wa baharini, mikoko na misitu.

Mbali na kutoa akiba ya masuluhisho ili kuwa maendeleo endelevu ya visiwa, mradi huu unalenga kuwezesha mataifa ya visiwa yanayokabiliwa na kupanda kwa viwango vya bahari na dhoruba zinazoongezeka kutokana mabadiliko ya tabianchi kusikika.

Mradi wa Kuhifadhi Mazingira wa Altyn Dala

Kama nyika nyingi kote ulimwenguni, nyika kubwa za Asia ya Kati zimepungua kutokana na sababu kama vile kulisha mifugo kupindukia, kubadilisha ardhi na kuifanya ya kilimo na mabadiliko ya tabianchi.   

Nchini Kazakhstan, ambapo Mradi wa Hifadhi ya Mazingira wa Altyn Dala umekuwa ukiendelea tangu mwaka wa 2005 kuboresha mifumo ya ekolojia ya maeneo ya nyika, maeneo kame na majangwa ndani ya maeneo ya kihistoria ya Saiga, eneo ambalo kuna wakati lilikuwa na swara waliokuwa hatarini kutokana na uwindaji na kupoteza makaazi.

Kwa hakika, idadi ya Saiga ilikuwa imepungua hadi 50,000 katika mwaka wa 2006 lakini ikaongezeka hadi milioni 1.3 kufikia mwaka wa 2022. Mbali na kuboresha na kulinda nyika, mradi huu umesaidia kuhifadhi ardhioevu ambayo ni kitovu muhimu kwa takriban ndege milioni 10 wa kuhamahama. Miongoni mwa aina kuu za ndege ni pamoja na lapwing, bata bukini aliye na wekundu, bata mwenye kichwa cheupe na korongo wa Siberia.

Eneo Kame la Amerika ya Kati

Eneo linalokabiliwa na mawimbi ya joto na mvua isiyotabirika, mifumo ya ekolojia na watu wa eneo kame la Amerika ya Kati iko hatarini zaidi kukumbwa na mabadiliko ya tabianchi. Hivi majuzi kama vile mwaka wa 2019, mwaka wa tano kwa mfulilizo wa ukame uliwaacha watu milioni 1.2 katika eneo wakihitaji msaada wa chakula.     

Kutumia mbinu za kijadi za kilimo ili kuboresha mandhari, ikiwa ni pamoja na bayoanuwai, ndicho kiini cha mradi huu unaojumuisha nchi sita:  Costa Rika, El Salvador, Guatemala, Honduras, Nicaragua na Panama.

Kwa mfano, mifumo ya kilimo cha misitu kinachojumuisha miti na mmea kama vile kahawa, kakao na iliki inaweza kuimarisha rutuba ya udongo na upatikanaji wa maji huku ikiendeleza bayoanuwai nyingi za msitu asilia ya maeneo ya tropiki. 

Kufikia mwaka wa 2030, lengo ni kuwa na hekta 100,000 ya miti na kubuni nafasi za kazi za kudumu 5,000.

Kushirikiana na Mazingira Nchini Indonesia 

Demak, jamii ya pwani ya maeneo ya chini kwenye kisiwa kikuu cha Java nchini Indonesia, imekumbwa na mmomonyoko wa udongo, mafuriko na haribifu wa ardhi kutokana na kuondolewa kwa mikoko ili kujenga mabwawa ya ufugaji wa samaki, kukuza chakula na kuweka miundomsingi. 

Badala ya kupanda tena miti ya mikoko, mradi huu mkuu bunifu wa kuboresha mifumo ya ekolojia umetumia nyenzo za kiasili kujenga vitu vilivyo na muundo wa ua kando ya ufuo ili kutuliza mawimbi na kunasa mashapo, na hivyo kutengeneza mazingira ya mikoko kuwepo tena. Urefu kwa jumla wa vitu vilivyojengwa ni kilomita 3.4 na hekta 199 za mikoko zimerejeshwa.    

Ili kuruhusu mikoko kuzaana, wakulima wamefundishwa mbinu endelevu ambazo zimeongeza uzalishaji wao wa kamba. Pamoja na mikoko kutoa makaazi kwa viumbe vingi vya baharini, kiwango cha samaki kinachovuliwa na wavuvi kimeongezeka.

Mradi wa Shan-Shui Nchini China

Mradi huu kabambe unajumuisha miradi mikubwa 75 ya kuboresha mifumo ya ekolojia, inayojumuisha milima, miamba ya pwani katika taifa lililo na idadi kubwa zaidi ya watu duniani.  

Mradi uloizinduliwa katika mwaka wa 2016, mradi huu unatokana na mikakati taratibu ya kuboresha mifumo ya ekolojia. Miradi inaambatana na mipango ya kitaifa ya anga, inafanya kazi katika mandhari au maeneo ya maji na inajumuisha maeneo ya kilimo na mijini pamoja na mifumo ya ekolojia ya kiasili, na inalenga kukuza tasnia nyingi ndani ya nchi hiyo. Yote ni muhimu kwa bayoanuai.

Mifano ni pamoja na Mradi wa Maji ya Mto Oujiang katika mkoa wa Zhejiang, unaojumuisha maarifa ya kisayansi na mbinu za kijadi za kilimo, kama vile kuweka matuta kwenye miteremko na kuchanganya kilimo cha mimea, samaki na ufugaji bata, ili kufanya matumizi ya ardhi kuwa endelevu zaidi.

Angalau hekta milioni 2 zimeboreshwa hadi sasa. Mradi unalenga kufikia hekta milioni 10 kufikia mwaka wa 2030.

Muongo wa Umoja wa Mataifa wa Kuboresha Mifumo ya Ekolojia unaendelea hadi mwaka wa 2030, ambayo pia ni makataa ya kufikia Malengo ya Maendeleo Endelevu. Bila kusitisha na kukabiliana na uharibifu wa mifumo ya ekolojia ya nchi kavu na majini, spishi milioni 1 ziko hatarini kutoweka.  Wanasayansi wanasema kuboresha asilimia 15 tu ya mifumo ya ekolojia katika maeneo yaliyopewa kipaumbele na hivyo kuboresha makaazi kunaweza kupunguza kutoweka kwa asilimia 60.

Muongo wa Umoja wa Mataifa unashughulikia Mikataba ya Rio yote mitatu na kuhimiza washirika wake kushirikisha utabiri wa hali ya hewa na mustakabali tofauti wa hali ya hewa katika juhudi zao za kuboresha mifumo ya ekolojia.

Hakujawahi kuwa na hitaji la dharura zaidi la kuboresha mifumo ya ekolojia iliyoharibiwa kuliko sasa. Mifumo ya ekolojia huwezesha maisha Duniani. Kadiri mifumo yetu ya ekolojia inavyoboreka, ndivyo sayari yetu na watu wake inavyoboreka. Uboreshaji wa Mifumo ya Ekolojia utafaulu tu ikiwa kila mtu atajiunga na vuguvugu la #GenerationRestoration ili kuzuia, kusitisha na kukabilianaa uharibifu wa mifumo ya ekolojia kote duniani.

 

MAKALA KWA WAHARIRI

Kuhusu Wabia wa kila mradi

Muungano wa Kutunza msitu wa Atlantiki Ulio katika Nchi Tatu

Mradi Huu Mkuu ya Kuboresha Mifumo ya Ekolojia Duniani Muungano wa Kutunza misitu ya Atlantiki Ilio katika Nchi Tatu na Mtandao wa Nchi Tatu wa Kuboresha Msitu wa Atlantiki.  Unapokea usaidizi kutoka kwa zaidi ya wabia 300, ikiwa ni pamoja na: Jumuiya ya Brazili ya Kuboresha Mifumo ya Ekolojia, Muungano wa Kimataifa wa Kuhifadhi wa MazingiraShirika la Kuhifadhi Mazingira nchini BraziliTaasisi ya Rasilimali Duniani Nchini BraziliMfuko wa Kimataifa wa Kufadhili Mazingira Nchini Brazili, na mashirika mengine mengi ya kimataifa na ya ndani ya nchi.

Kuboresha Ekolojia ya Maeneo ya Bahari Ncini Abu Dhabi,  Milki ya Falme za Kiarabu

Mradi Huu Mkuu ya Kuboresha Mifumo ya Ekolojia Duniani unaratibiwa na Shirika la Mazingira – Abu Dhabi.

Ukuta Mkubwa wa Kijani kwa Uboreshaji wa Mifumo ya Ekolojia na kwa amani

Mradi Huu Mkuu ya Kuboresha Mifumo ya Ekolojia Duniani unaratibiwa na Shirika la Kiafrika la Mradi wa Ukuta Mkubwa wa Kijani,  Mradi wa Ukuta Mkubwa wa Kijani katika Eneo la Sahara na Sahel, Shirika la Mradi wa Ukuta Mkubwa wa Kijani Nchini Nigeria, Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa, Mradi wa Ufadhili wa Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa, Kichocheo cha Mradi wa Ukuta Mkubwa wa Kijani - Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Kupambana na Kuenea kwa Majangwa, Kituo cha Utafiti wa Misitu wa Kimataifa, Jukwaa la Mazingira Duniani  na  Shirika la Chakula Duniani.

Namami Gange:

Mradi Huu Mkuu wa Kuboresha Mifumo ya Ekolojia Duniani unaratibiwa na Serikali ya India na Mpango wa Namami Gange kwa ushirikiano na Shirika la Maakazi ya Binadamu la Umoja wa Mataifa, Benki yaDunia, Taasisi ya Rasilimali Duniani  na Shirika la Maendeleo la Ujerumani.

Mradi wa kuboresha mifumo ya ekolojia ya nchi mbalimbali za maeneo ya milima

Mradi Huu Mkuu ya Kuboresha Mifumo ya Ekolojia Duniani unaratibiwa na Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa, Mkataba wa Carpathian na Ubia wa Maeneo ya Milima.

Mradi wa Kuboresha Mifumo ya Ekolojia katika Nchi za Visiwa Vidogo

Mradi Huu Mkuu ya Kuboresha Mifumo ya Ekolojia Duniani unaratibiwa na Serikali ya Comoros, Serikali ya Saint Lucia, Serikali ya Vanuatu, Muungano wa Kutunza Mazingira wa Nchi Zinazoendelea za Visiwa Vidogo, Idara ya Umoja wa Mataifa ya Masuala ya Kiuchumi na Kijamii, Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa, na Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa.

Mradi wa Kuhifadhi Mazingira wa Altyn Dala

Mradi Huu Mkuu ya Kuboresha Mifumo ya Ekolojia Duniani unaratibiwa na Muungano wa Kazakhstan wa Kuhifadhi Bayoanuai, Wizara ya Ekolojia, Jiolojia na Malighafi ya Jamhuri ya Kazakhstan, , Shirika la Kimataifa la Fauna & Flora, Jumuia ya Frankfurt ya Zoolojia, Jumuiya ya Kifalme ya Kutunza Ndege  na Mpango wa Uhifadhi wa Cambridge.

Urejeshaji wa Kilimo cha Misitu katika eneo kame la Amerika ya Kati:

Mradi Huu Mkuu ya Kuboresha Mifumo ya Ekolojia Duniani unaratibiwa na Tume ya Amerika ya Kati ya Mazingira na Maendeleo, Baraza la Kilimo la Amerika ya Kati, Mfumo wa Ushirikiano wa Amerika ya Kati, Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa, Mfuko wa Mazingira ya Kijani, Serikali ya El Salvador, Kituo cha Ushirikiano cha Utafiti wa Kimataifa wa Misitu na Muungano wa Kimataifa wa Kuhifadhi Mazingira.

Kushirikiana na Mazingira nchini Indonesia - Kuboresha ufuo unaomomonyoka na kuchochea uchukuaji wa hatua kwa kiwango kikubwa:

Mradi Huu Mkuu ya Kuboresha Mifumo ya Ekolojia Duniani unaratibiwa na Wizara ya Mambo ya Bahari na Uvuvi  ya Indonesia, Wizara ya Kazi ya Umma na Makazi ya Indonesia, Ardhioevu ya Kimataifa na Ecoshape kwa ushirikiano naWitteveen + BosDeltaresTU DelftChuo Kikuu cha Wageningen & Utafiti,UNESCO-IHEBlue ForestsKota KitaVon LiebermanChuo Kikuu cha Diponegoro, na jamii za wenyeji.

Mradi wa Shan-Shui nchini China

Mradi Huu Mkuu ya Kuboresha Mifumo ya Ekolojia Duniani unaratibiwa na Wizara ya Malighafi naWizara ya Fedha, Jamhuri ya Watu wa China na msaada mkubwa kutoka kwa idara zinazohusiana na serikali za mitaa.

Mradi Mkuu wa Kuboresha Mifumo ya Ekolojia Duniani ni nini? 

Nchi tayari zimeahidi kuboresha hekta bilioni 1 za ardhi - eneo kubwa kuliko Uchina – kama sehemu ya ahadi zao kwa Mkataba wa Paris wa mazingira, malengo ya Aichiya bayoanuai, malengo ya Kukomesha Uharibifu wa ArdhinaMalengo ya Bonn. Hata hivyo, mengi hayajulikani kuhusu hatua zilizopigwa au kiwango cha ubora cha miradi hii. Hatua za miradi yote 10 ya Kuboresha Mifumo ya Ekolojia Duniani zitafuatiliwa kwa njia ya uwazi kupitia Mfumo wa Ufuatiliaji wa Uboreshaji wa Mifumo ya Ekolojia, jukwaa la Muongo wa Umoja wa Mataifala kufuatilia juhudi za uboshaji wa nifumo ya ekolojia kote duniani.

Kupitia Miradi Mikuu ya Kuboresha Mifumo ya Ekolojia Duniani, Muongo wa Umoja wa Mataifawa Kuboresha Mifumo ya Ekolojia unalenga kutuza mifano bora ya kuigwa ya uboreshaji wa mifumo ya ekolojia kwa kiwango kikubwa na kwa kipindi kirefu katika nchi yoyote na eneo lolote, kwa kuzingatia Kanuni 10 za Uboreshaji wa Mifumo ya Ekolojia za Muongo wa Umoja wa Mataifa. 

Kuhusu Muongo wa Umoja wa Mataifa wa Kuboresha Mifumo ya Ekolojia 

Baraza la Umoja wa Mataifa lilitangaza kuanzia mwaka wa 2021 hadi mwaka wa 2030  Muongo wa Umoja wa Mataifa wa Kuboresha Mifumo ya Ekolojia. Unaongozwa na Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa na Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa kwa ushirikiano na wabia. Ulizinduliwa ili kuzuia, kusitisha na kukabiliana na udidimiaji na uharibifu wa mifumo ya ekolojia kote ulimwenguni.  Unalenga kuboresha mamilioni ya hekta ya ardhi katika mifumo ya ekolojia ya nchi kavu na majini.  Ni wito wa kuchukua hatua za kimataifa, Muongo wa Umoja wa Mataifa huungwa mkono wa wanasiasa, utafiti wa kisayansi, na wafadhili ili kuimarisha uboreshaji wa mifumo ya ekolojia kwa kiwango cha juu. 

Kuhusu Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEP)
UNEP ni mhamasishaji mkuu wa masuala ya mazingira duniani. Hutoa uongozi na kuhimiza ushirikiano katika utunzaji wa mazingira kupitia kwa kuvutia, kuelimisha na kuwezesha mataifa na watu kuimarisha maisha yao bila kuhatarisha yale ya vizazi vijavyo.    

Kwa maelezo zaidi, tafadhali wasiliana na:  

Moses Osani, Afisa wa Vyombo vya Habari, Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa