Photo by UNEP
30 Mar 2021 Tukio Kutumia mazingira kushughulikia tabianchi

Programu mpya ya kusaidia pwani ya Kenya na uchumi wa maeneo ya bahari

Photo by UNEP

Kikosi cha Ulaya, kwa ushirikiano na Magavana wa kaunti sita za pwani nchini Kenya, Wizara ya Ugatuzi na Sekretarieti ya Uchumi wa Maeneo ya Bahari, walizindua mradi wa Go Blue nchini Kenya tarehe 25 mwezi wa Machi mwaka wa 2021. Programu hiyo ya miaka minne inakusudia kutunza mazingira ya pwani ya Kenya huku ikibuni nafasi za kazi zinazojali mazingira katika sekta mbalimbali, ikijumuisha kuunda bidhaa kwa vitu vilivyotumika, utalii na uvuvi mdogomdogo. Imeundwa kukuza "uchumi endelevu wa maeneo ya bahari" katika kaunti sita za pwani na kutoa zaidi ya ajira 3,000 kwa vijana na wanawake tu.

Go Blue imepokea yuro milioni 25 kama ufadhili kutoka Muungano wa Ulaya. Nchi nne wanachama wa Muungano wa Ulaya (EU) - Ufaransa, Ujerumani, Italia, na Ureno - zitatoa maarifa ya kiufundi kuhusu ukuaji wa uchumi, huku mashirika mawili ya Umoja wa Mataifa - Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEP) na  UN-Habitat - watahakikisha kuwa hatua zitakazochukuliwa zitafungamanishwa na uhifadhi wa mazingira na malengo ya upangaji wa miji na kuwa programu hiyo itasaidia miji na jamii za pwani kukabiliana na athari mbaya za mabadiliko ya tabianchi.

 "Mifumo yetu ya maeneo ya baharini na pwani ni muhimu sana katika utoaji wa huduma za mifumo ya ekolojia - huku watu wengi wakipata riziki kupitia mifumo hiyo," alisema Inger Andersen, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEP). "Badala ya kumaliza au kuchafua rasilimali hizi, lazima tubuni njia za kuzitumia na kuzitunza."

Hatua hizi zinahitajika katika mazingira ya baharini kote ulimwenguni, ikijumuisha yale ya Kenya, yanayokabiliwa na shinikizo kubwa kutokana na mabadiliko ya tabianchi na uchafuzi.  

Kenya ina rasilimali nyingi za baharini ambazo hazijatumika katika maeneo ya pwani. Go Blue inalenga kusaidia jamii za pwani kukuza rasilimali hizo kwa njia ambayo ni endelevu na ambayo inatoa fursa za kiuchumi kwa wanawake na vijana. Mradi huo utatumia njia shirikishi, jumuishi na endelevu kukuza uchumi, huku ukibuni nafasi mpya za kazi, kama vile uvuvi mdogomgogo, kuunda vitu kutoka kwa taka, ufugaji wa wanyama na mimea ya majini au utalii, na maarifa ya kiufundi katika sekta za uchumi wa maeneo ya baharini, kuimarisha usambasaji wa bidhaa na kukabiliana na vikwazo vya kikanda.

Pia utaimarisha juhudi za kaunti za pwani za kubuni mikakati za upangaji na usimamizi wa maeneo ya ardhi na baharini kwa lengo la kuboresha mifumo muhimu ya ekolojia ya maeneo ya pwani na bahari. Mwishowe, Walinzi wa Maeneo ya Pwani nchini Kenya watajengewa uwezo ili kulinda rasilimali za bahari.

"Kufanya kazi kwa pamoja ili kupata masuluhisho- kwenye maeneo ya ardhi na majini-katika ngazi mbalimbali serikalini na kwa kuzingatia sekta mbalimbali ni muhimu ili kuwa na uchumi endelevu wa maeneo ya bahari," alisema Maimunah Mohd. Sharif, Mkurugenzi Mtendaji wa UN-Habitat.

Go Blue itatekelezwa kwa kushirikiana na Jumuiya ya Kaunti za Pwani - Shirika la Maendeleo ya Uchumi wa kaunti za mkoa wa pwani wa Kenya - kwa ushirikiano na wizara za kitaifa, kama vile Sekretarieti ya Uchumi wa Maeneo ya Bahari, Wizara ya Kilimo na Uvuvi, Huduma ya Walinzi wa Pwani ya Kenya, Wizara ya Mambo ya Ndani , Wizara ya Uchukuzi na Chuo cha Bandari Maritime Academy.

UN-Habitat na UNEP zitasaidia kaunti sita kubuni methodolojia tatu:

  • mfumo jumuishi wa upangaji na usimamizi wa maeneo ya ardhi na bahari, utakaoboresha upangaji wa anga
  • maono ya kikanda kuhusiana na maeneo ya ardhi na bahari ya kutoa kipaumbele kwa maswala yanayohusiana na uchumi wa maeneo ya bahari.
  • ubadilishanaji wa data, ukusanyaji wa data na uchambuzi wa upangaji wa anga na tathmini ya mifumo ya ekolojia

Hii itatumiwa kwenye maabara ya GIS ya data kaunti ya, na pia kwenye kitovu cha GIS cha data ya ukanda , kuimarisha ukusanyaji na uchambuzi wa mabadiliko ya matumizi ya ardhi, miji na mabadiliko ya mazingira, malighafi ya baharini na pwani, na shughuli za binadamu (mfano uvuvi, utalii , taka). Kwa kuongezea, mradi huo utasaidia usimamizi wa taka, maeneo oevu yaliyojengwa, hewa ya ukaa kutoka baharini, upandaji wa mikoko, upangaji wa anga na kujengea jamii uwezo.

Habari na ushahidi kutoka kwa shughuli zote zitawezesha uigaji katika miji mingine ya Kenya kupitia jukwaa la kugawana maarifa na mafunzo mtandaoni . Kwa kuongezea, kaunti nne zinapaswa kuunda mapendekezo yao ya upangaji wa maeneo ya ardhi na bahari kutokana na mradi huo, na shughuli sita za ubunifu zitafadhiliwa na wawekezaji ambao wanachangia moja kwa moja kwa uchumi wa bahari na upangaji maeneo ya bahari